Bunge la Kenya limeidhinisha kuondolewa kwa Naibu wa Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua katika nafasi hiyo baada ya Wabunge 281 kati ya 325 kupiga kura ya kusema aondoke kutokana na tuhuma mbalimbali ikiwemo ya kujitajirisha na kuibua chuki za kikabila.

Baada ya kura hizo, hatua inayofuata ni hoja hiyo kupelekwa kwenye Bunge la Seneti ambapo ikiidhinishwa huko, Gachagua atakuwa Naibu wa kwanza wa Rais kuondolewa madarakani Nchini Kenya.

Akiwa na ripoti ya kurasa 500, Gachagua ambaye anadai kuchafuliwa na kashfa hizo alifika mbele ya Baraza la Mawaziri wakati wa kikao cha Bunge cha saa 12 kilichokuwa kikali ambapo pamoja na yeye kukana mashtaka dhidi yake, Wabunge wengi wamepiga kura wakitaka aondoke.

Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangula sasa ana siku mbili za kumjulisha Mwenzake wa Seneti Amason Kingi ambapo atatakiwa kuitisha kikao cha Seneti ndani ya siku saba kuchunguza mashtaka dhidi ya Gachagua ambapo kwa mujibu wa Katiba, Seneti itaunda Kamati Maalum ya Wanachama 11 kuchunguza madai hayo ndani ya siku saba na baadaye Kamati hii itaripoti matokeo yake kwa Seneti ndani ya siku 10 ambapo Gachagua pia ataitwa yeye binafsi au kuwakilishwa mbele ya kamati maalum wakati wa uchunguzi wake.

Kifungu cha 145 cha katiba hiyo ya mwaka 2010 kinasema iwapo madai hayo yatathibitishwa, Seneti itapiga kura kwa kila shtaka la kumshtaki na ikiwa angalau theluthi mbili ya Wanachama wote wa Seneti watapiga kura kuunga mkono mashtaka yoyote ya kushtakiwa, Gachagua ataachia ngazi na kushtakiwa.

By Jimmy

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *